Mfuko wa Maendeleo ya Jamii nchini TASAF umeendelea na utaratibu wake wa kuwakutanisha watendaji wake ngazi ya Halmashauri za wilaya na Waandishi wa habari kwa lengo la kujenga uelewa juu ya mpango wa kunusuru kaya Masikini ili kuwawezesha waandishi hao kuujua ipasavyo .
Akifungua kikao kazi hicho kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, bwana Ladislaus Mwamanga ,Mkurugenzi wa Ukaguzi wa TASAF Bwana Christopher Sanga ameelezea mafanikio yaliyokwishaanza kuonekana kupitia utekelezaji wa Mpango huo kuwa yanaonyesha umuhimu wa Mpango huo katika vita dhidi ya umasikini nchini.
Amesema walengwa wa Mpango wa Kunusuru kaya Masikini ambao wamenufaika na ruzuku kupitia Mpango huo wameanza kupata mabadiliko hususani katika kujenga uwezo wa kuwasomesha watoto wao,kugharamia huduma za matibabu, kuboresha lishe na hata kuongeza vipato yao ikiwemo ufugaji wa kuku,mbuzi n.k.
Tayari vikao kazi hivyo vimefanyika katika miji ya Arusha,Morogoro,Njombe, Mtwara, Tanga, Kigoma na Mwanza ambapo waandishi mbalimbali wameshiriki na kuweka mkakati wa kufanya kazi na TASAF katika kuutangaza Mpango wa Kunusuru kaya Masikini uliozinduliwa na Rais Jakaya Kikwete mjini Dodoma Agosti 2012.
Zifuatazo ni baadhi ya picha za washiriki wa kikao kazi hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Nyakahoja jijini Mwanza.
Mkurugenzi wa kujenga uwezo wa TASAF, Bwana Farij Mishael aliyesimama akizungumza katika kikao kazi cha watendaji wa TASAF na waandishi wa habari kushoto kwake ni Mkurugenzi wa ukaguzi wa Christopher Sanga , na kulia kwake ni Kaimu Mkurugenzi wa Fedha Bwana Njego Nyamuko
Mkurugenzi wa ukaguzi wa TASAF Bw. Christopher Sanga aliyesimama , akifungua kikao kazi cha watendaji wa TASAF kutoka mikoa ya Kagera.Geita na Shinyanga ,Kulia kwake ni Mkurugenzi wa kujenga uwezo Bwana Farij Mishael akifuatiwa na Kaimu mkurugnezi wa fedha Njego Nyamuko
Baadhi ya washiriki wa kikao kazi cha watendaji wa TASAF wakimsikiliza Mkurugenzi wa ukaguzi Christopher Sanga hayupo pichani wakati alipofungua kikao kazi hicho.
Baadhi ya washiriki wa kikao kazi cha watendaji wa TASAF na waandishi wa Habari kutoka mikoa ya Geita,Shinyanga na Kagera wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa TASAF .