Waziri wa nchi Ofisi ya Rais Uratibu na Mahusiano,Mheshimiwa Dokta Mary Nagu amepongeza hatua iliyofikiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF, katika kutekeleza sera ya kupambana na umaskini na kutatua kero zinazowasibu wananchi.
Dokta Nagu ameyasema hayo alipotembelea makao makuu ya TASAF jijini Dar es salaam ikiwa ni mwendelezo wa ziara ya kutembelea taasisi za serikali anazoziongoza kufuatia mabadiliko ya baraza la Mawaziri yaliyofanywa na Rais Dokta Jakaya Kikwete hivi karibuni.
Ametoa mfano wa utekelezaji wa miradi ya TASAF tangu kuanzishwa kwake karibu miaka 15 iliyopita kuwa kiasi cha shilingi bilioni 541 zimetumika jambo ambalo amesema limechangia kwa kiwango kikubwa kuleta maendeleo na kuibua miradi ya kiuchumi kwa wananchi.
Waziri huyo amewataka watumishi wa TASAF waendelee kutekeleza majukumu yao kwa kujituma zaidi huku wakizingatia utoaji wa huduma kwa wananchi itakayosaidia kuboresha maisha yao.
Aidha Dokta Nagu ametaka TASAF kuweka mkakati mahususi wa kukuza vikundi vya kuweka akiba VICOBA ambavyo amesema vimeonyesha mafanikio makubwa katika maeneo ambako vinaendeshwa.
Akitoa maelezo ya utekelezaji wa shughuli za TASAF ,Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko huo ,Bwana Ladislaus Mwamanga amesema tangu kuanzishwa kwake Taasisi hiyo imepata mafanikio makubwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa majengo ya madarasa,zahanati,maji,na miradi ya hifadhi ya mazingira katika maeneo kadhaa nchini .
Bwana Mwamanga pia amesema hatua muhimu imefikiwa katika kutekeleza Mpango wa Kunusuru kaya maskini, PSSN na kuwa ifikapo mwezi Juni Mwaka huu walengwa wa Mpango huo watakuwa wamefikiwa kote nchini. Hadi sasa kiasi cha takribani shilingi Bilioni 40 kimelipwa kwa kaya maskini tangu utekelezaji wa Mpango huo uanze.
Karibu TASAF hivyo ndivyo anavyoelekea kusema mkurugenzi Mtendaji wa TASAF,Ladislaus Mwamanga alipomkaribisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Dokta Mary Nagu ambaye amefanya ziara ya kujitambulisha katika taasisi hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Ladislaus Mwamanga akimtembeza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Dokta Mary Nagu katika jengo linalotumiwa kuhifadhi kumbukumbu za walengwa wa Mpango wa Kunusuru kaya maskini.
Waziri wa nchi ofisi ya Rais Dokta Mary Nagu akzungumza na menejimenti ya TASAF katika ziara yake katika taasisi hiyo .
Waziri wa nchi ofisi ya Rais mahusiano na uratibu Dokta Mary Nagu (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na menejimenti ya TASAF kushoto kwake ni mkurugenzi mtendaji wa TASAF Ladislaus Mwamanga (mwenye suti nyeusi)